Ufafanuzi Wa 'Aqiyqah Anayofanyiwa Mtoto Mchanga Katika Sunnah
‘Aqiyqah maana yake ni kukata. Na katika sharia ni mbuzi anayechinjwa kwa ajili ya mtoto aliyezaliwa anapofika siku ya saba tokea kuzaliwa kwake.
‘Aqiyqah ni Sunnah iliyotiliwa mkazo kwa mwenye uwezo nayo.
Na hili ni jukumu la wazazi kumfanyia mtoto wao kwa kauli ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)
“Kila mtoto amefungika na ‘Aqiyqah yake, itachinjwa kwa ajili yake siku ya saba na atapewa jina, na atanyolewa kichwa chake” (Ahmad na An-Nasaaiy).
Kwa ajili ya shughuli hiyo ni lazima achinjwe mnyama anayefaa kuchinjwa kwa ajili ya Udh-hiyah kwa kuzingatia kusalimika kwake na kasoro yoyote kama kuwa kilema au kukosa jicho na umri wake uwe zaidi ya mwaka.
Baada ya kuchinjwa mnyama huyo akiwa ni mbuzi au kondoo ni Sunnah kumgawa kama inavyogaiwa nyama ya Udh-hiyah. Baadhi ya nyama watakula watu wa nyumbani, na nyingine utatoa sadaka.
Ni vyema na ndio sahihi zaidi kuchinja siku ya 7 ama riwaya za siku ya 14 au 21 au 28 hazina uhakika sana. Kwa hiyo mtu ajihimu sana kuchinja siku hiyo ya saba. Ikiwa hakuweza kwa sababu fulani fulani, basi Maulamaa wanasema kuwa anaweza kufanya wakati wowote katika uhai wake.
‘Aqiyqah ya mtoto wa kiume ni mbuzi wawili na wa kike ni mbuzi mmoja kama alivyofanya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):
“Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alichinja mbuzi wawili alipozaliwa Hassan” (At-Tirmidhiy).
Japokuwa zipo riwaya nyingine ambazo zinaonyesha kuwa mtoto wa kiume na wa kike wanachinjiwa mbuzi mmoja mmoja.
Wanachuoni wamekanusha riwaya hizi kwa kusema ni vyema kwa mvulana kuchinjiwa mbuzi wawili lakini ikiwa mzazi hana uwezo basi atachinja mmoja.
Ikiwa mtoto atakufa kabla ya siku ya saba basi hatochinjiwa..