MALAIKA SEHEMU YA 2
ALIMJARIBU 'BOI' WA NDANI ILI KUHAKIKISHA KAMA NI TASA
Hapo ndipo Malaika alipohisi dunia nzima imemuelekea yeye. Kila kona aliyopita ilikuwa ni masengenyo, dharau za ndugu, na minong’ono ya majirani iliyomchoma kama mkuki. Lakini kilichokuwa kinamuua kabisa ni Baraka, mume wake. Yule mwanaume aliyemwahidi kumlinda "kwenye shida na raha," sasa amekuwa baridi kama barafu, anampuuza na kumtazama kama vile yeye ndiye balaa lililoingia kwenye ile nyumba ya Arusha.
Ile hali ya kuishi na mume ambaye hakuongeleshi, anakukasirikie bila sababu, na kukuona huna thamani, ilimvua nguvu Malaika. Alikuwa anatembea ndani ya lile jumba kama msukule; kuta za nyumba zilionekana kama zinataka kummeza. Kila akiona watoto wa majirani wakicheza nje, alihisi kisu kinapita moyoni mwake. Alijiona kama mti uliokauka katikati ya bustani ya tajiri—huna faida, huna matunda.
Siku moja mchana, hali ya hewa ilikuwa imetulia tuli. Baraka alikuwa kazini, na ndani kulikuwa na Malaika na Sule, yule kijana wa kazi. Malaika alikuwa sebuleni, akipandisha vinywaji vikali ili angalau asahau machungu yake. Hapo ndipo wazo la "kichaa" likamjia kichwani—wazo ambalo mwanamke mwenye akili timamu hawezi kulifikiria, lakini kukata tamaa kulimfanya aone ni sawa.
“Siku zangu za hatari (Ovulation) ni sasa... Je, nikimjaribu Sule? Si nitapata jibu kama kweli mimi ni tasa au la?”
Moyo ulimlipuka kwa kasi! Alijua ni dhambi, alijua ni hatari, lakini alihitaji jibu, na labda pia alitaka kulipiza kisasi kwa dharau za mume wake. Akajikaza, akamwita Sule kutoka uani.
“Sule! Njoo huku ndani mara moja.”
Sule akaingia huku anafuta jasho, “Naam, Ma.”
“Niletee chupa nyingine ya mvinyo hapa,” Malaika alisema huku anajidai mchangamfu. Alipoileta, Malaika akamkaribisha na yeye. “Chukua glasi hii, kunywa kidogo na mimi.”
Sule alishtuka, akachezesha macho. “Samahani Madam... kwani kuna sherehe gani leo?”
“Hakuna sherehe mwanangu, nimeamua tu kunywa, na kunywa peke yangu ni upweke mtupu.”
“Ah Madam, mimi hizi pombe za kizungu zinanipiga chenga sana.”
“Hunywi kabisa?”
“Nakunywa bia kidogo, lakini hizi zingine hapana.”
Malaika akacheka kidogo, “Basi jaribu hii kidogo tu. Lakini kabla ya hapo, nenda duka la dawa hapo mbele ukaninunulie kitu.”
Aliandika jina la dawa fulani kwenye karatasi—dawa ambayo inatuliza mwili lakini inaongeza msisimko na hamu. “Wakiuliza ya nini, sema unataka kitu cha kuuweka mwili sawa, usitoe maelezo mengi. Na usiende famasi kubwa, nenda hapo chemist ya mtaani haraka.”
Sule akatii, akatoka. Malaika alibaki anatetemeka. Hakujua kama anachofanya ni ujasiri au ni ukichaa uliopitiliza. Baada ya dakika kadhaa, Sule akarudi na ile dawa. Malaika akaipokea, kisha akamtuma Sule akakague kama geti limefungwa vizuri. Sule alipotoka tu, Malaika akamimina kile kichocheo kwenye kinywaji cha Sule na kukikoroga kwa umakini.
“Wacha nione kama atahimili huu mlegezo,” aliwaza.
Sule alirudi, Malaika akamwambia, “Funga mlango vizuri, piga na kufuli kabisa kwa usalama wetu.” Sule alitii bila kujua kinachoendelea. Alipoketi, Malaika akamlazimisha kunywa kile kinywaji, akamsaidia kabisa mpaka akamaliza.
Saa moja halikuisha, Sule akaanza kulegea. Macho yakawa mazito, maneno yakawa yanatoka kwa shida, mwili ukamshinda kabisa. Alikuwa kama mtu aliyepagawa na usingizi mzito na ulevi wa ghafla. Malaika, kwa sababu ya upofu wa mawazo yake, aliona huo ndio muda wa kufanya kile "jaribio" lake. Sule hakuwa na uwezo wa kukataa wala kuelewa kinachoendelea; alikuwa kama amepoteza fahamu huku Malaika akiongoza kila hatua.
Baada ya mchezo kuisha, Sule alisinzia fofofo pale pale kwenye kochi. Malaika akafanya usafi wa haraka sebuleni, akahakikisha kila kitu kipo sawa kama hakuna kilichotokea.
Baada ya masaa mawili, Baraka alirudi kutoka kazini. Akamkuta Sule amelala fofofo sebuleni.
“Huyu kijana ana nini? Mbona amelala hapa kama amekufa?” Baraka aliuliza kwa mshangao.
“Atakuwa amechoka tu mume wangu,” Malaika alijibu kwa utulivu wa ajabu. “Nimempa kazi nyingi sana leo, labda yamemchosha.”
“Haya, kama unasema hivyo, sawa.”
Sule alikuja kushtuka baadaye, kichwa kinamuuma kama kimepasuliwa na kizunguzungu cha ajabu. Hakuwa anakumbuka chochote cha maana. Madam alimpakulia chakula, naye akaenda chumbani kwake (boy’s quarters) kulala tena.
Malaika akajihisi ana amani fulani hivi ya ajabu. Aliona kama amemkomoa Baraka na dharau zake. Alijidanganya kuwa amefanya jambo sahihi.
Lakini maskini, hakujua kuwa lile tukio la alasiri ile litaenda kubadilisha maisha yao milele. Miezi michache mbele, siri hiyo ingeleta maswali ambayo yangemvua nguo si tu Malaika, bali hata Baraka mwenyewe na uanaume wake anaoujivunia.
ITAENDELEA...
Makala nyingine zinazocheza na ladha yako
Mapendekezo haya yanatokana na kile unachosoma sasa + Endelea kugundua zaidi
Maoni