SIMULIZI: LUCKY (SIHITAJI KURUDI NILIKOTOKA)
SEHEMU YA 01
Mwaka mmoja ukiwa umepita tokea binti mwenye umri wa miaka 24 Lucky ajiunge na chuo kikuu cha Dar es salam ( University of Dar es salam ) maarufu kama UDSM. Marafiki zake aliokuwa anakaa nao chumba kimoja katika vyumba vya kulala wanafunzi chuoni hapo, waliojulikana kwa majina ya Mariam, Tunu na Amina. Asubuhi na mapema ya siku ya wikiend ya jumamosi waliamua kumkalisha chini rafiki yao huyo kwa ajili ya kuongea naye mambo flani mawili matatu kutokana na jinsi walivyokuwa wanaishi naye katika hali ya unyonge na kuonekana hapendi kushirikiana na mtu yoyote kimasomo hadi starehe za hapa na pale.
Maisha waliyoishi naye yalikuwa yanawatatiza, yanawakosesha raha. Waliishi naye kama sio mwenzao, walipohitaji ushirikiano wake hakuhitaji kuwa nao, muda mwingine walimshuhudia akikaa kiupweke hadi kutoa machozi kwa muonekano wa kuwaza mambo mazito aliyonayo moyoni mwake, walimuonea huruma hasa kwa sababu wao ni watu waongeaji wacheshi wa muda wote. Walimkalia vikao vya kimya kimya walipopata nafasi ya kipeke yao, lakini namna siku zilivyozidi kwenda mbele ndivyo Lucky alizidi kutia huruma na kuishi katika mazingira ya kuusononesha uso wake, uvumilivu uliwashinda na kuamua kumkalisha chini ikiwezekana awaambie chochote kinachomsumbua moyoni mwake huenda wakawa na ushauri wa kumshauri au wakampatia msaada uliopo ndani ya uwezo wao.
"Lucky mpenzi kikao hichi ni kwa ajili yako, tumeacha shughuli zetu ili tuongee na wewe. Tumeishi hapa mwaka sasa, lakini mwenendo wako na wetu ni vitu viwili tofauti, kuna muda tumekushuhudia ukimwaga machozi bila sababu, mawazo yasiyoisha, huzuni wasiwasi na vyengine kama hivyo, vitu ambavyo vimetushinda kuvivumilia kiukweli, kwa sababu sisi wakati wote ni watu wa kufurahi, kucheka. Kununa na kukasirika sisi hatujui Lucky. Tunaumia sana tunapoona mwenzetu tunayeishi naye chumba kimoja haupo kama sisi, huoneshi furaha hata siku moja, tunaomba utueleze kitu gani hasa kinasumbua maishani mwako tafadhali huenda ikawa njia ya kuondokana na hiyo hali inayokutatiza muda mwingi bila shaka"
Tunu aliyekuwa pembeni yake alimuuliza akiwa amemuangalia kwa kushika mkono kwenye tama, Lucky mwenyewe alishikilia mto uliokuwa mapajani mwake machoni akionesha hayupo nao, Mariam na Amina walikuwa wamekaa katika kitanda cha pili wakimtizama kwa macho yasiyoisha huruma.
"Tunaomba utuambie kitu gani kinakusumbua maishani mwako sisi ni marafiki wema, au tokea uingie hapa kuna jambo lolote baya tumekufanyia linalokufanya uwe hivyo?" Aliuliza Tunu Lucky akatingisha kichwa kuashiria hamna. " Sasa kwa nini unatufanyia hivyo hatupendi sisi Lucky, tuambie nini kinakusumbua hatuhitaji uwe katika hali hiyo"
" Hapana Tunu mimi sina tatizo lolote" Alisema Lucky baada ya kupitisha mkono machoni kufuta machozi yaliyokuwa tayari yanamlenga.
"Lucky unajaribu kuficha ugonjwa usiofichika, hapo tu tayari machozi yanakutoka kisha unasema huna tatizo? Tupo wanne tu hapa, zaidi yetu hakuna mwengine anayetuona wala kutusikia tuambie tafadhali" Alisema Mariam ambaye walipendelea sana kumuita Baby Merry.
"Mtoto koma mwengine yupo anayetusikia" Amina Alidakia maneno ya Mariam.
"Ushaanza nani anatuona hapa?" Aliuliza Mariam kwa kushtuka, Amina kidogo alikuwa shambenga asiyetaka kitu kimpite.
"Sir God, anaona hadi uvunguni kama hujui"
"Nilijua tu utasema hivyo, usilete matani wakati tupo ndani ya serious issue bhana, unaichukulia baridi hali ya mwenzetu?"
"Hapana kazi na dawa, kucheka kidogo kununa kidogo maisha yanaenda, baby Lucky tunaomba utuambie basi kitu gani kinakusumbua mamy, ujue kukaa na tatizo moyono si kutatua tatizo ee." Alisema Amina.
"Sina tatizo mimi Amina nipo kawaida."
"Tatizo unalo, ujue hapa chuoni kuna kamchezo kabaya kanaendelea japo kwa upande mwengine kazuri, tukikuona hivyo hatukuelewi tutaenda kushtaki kwa kiongozi wa chuo, bora utuambie sisi mpenzi umbea utabaki humu humu ndani" Alisema Amina huku akiwa amewaangalia wenzake.
"Nawaomba hali yangu msimwambie mtu yoyote, sihitaji watu wajue ninavyoishi tafadhali, haya ndio maisha yangu tokea nipo nyumbani" Alisema Lucky akiwa ameangalia chini, waliendelea kumshawishi ili awaambie kile walichokuwa wanakihisi toka kwake lakini wapi, mwisho waliamua kuachana naye wakimsihi sana abadilike laa sivyo watashindwa kuishi naye, upweke anaoweka hawauwezi kutokana na jinsi walivyozoea kucheka na kila mmoja.
Siku zilisonga mbele maisha ya Lucky yakiwa hayo hayo ya ukimya, muonekano wa msongamano wa mawazo na kujipwekesha na wenzake, ilifika sehemu wenzie anaolala nao walichoka ikabidi wamfate tena kumuweka chini lakini hakuna kilichobadilika. Jinsi alivyokuwa anakaa alifanana na msaka tonge anayesaka tonge lake katika wakati mgumu, wakati anatoka moja ya familia za kitajiri mno jijini Dar es salam.
Alivyoishi chuoni hapo Lucky. Aliwachukiza tu wale anaoishi nao chumba kimoja ila walimu wengi walitokea kumpenda na kumjumuisha katika daftari la wanafunzi bora mfano wa kuigwa na kila mmoja. Kipindi chote cha mwaka mzima alibahatika kupokea tuzo ya mwanafunzi msafi na mwenye nidhamu kuliko wote, hakuna alichoambiwa na walimu afanye akakataa labda kiwe kibaya, alikuwa mtiifu kuliko watiifu, upole huruma kwa wanafunzi wenziwe pamoja na muonekano wa kudeal na masomo wakati wote hata alipokuwa chumbani.
Wengi walipendelea mambo ya michezo wanapokuwa hawana ratiba yoyote ya masomo, au kutumia muda huo kwenda kula bata sehemu mbali mbali maclub na kwengine, lakini yeye aliutumia muda huo kupitia vitabu mbali mbali, baadhi ya wanafunzi wakawa wanamuonea wivu.
Tabasam kwake ndio kilikuwa kicheko, tofauti na wengine. Hakuna alichokihitaji zaidi ya kusoma, pale alipochoka alipanda kitandani kulala, lakini moja ya kawaida yake ambayo anao lala nao waliizoea, hawezi kulala mpaka machozi ya mawazo yamtoke, kitu kilichopelekea waamini huenda alipitia kipindi kigumu cha maisha ndio maana analia kila wakati, na ana maisha magumu kupita maelezo. Jambo ambalo lilikuwa sio sahihi.
Hakuna aliyeweza kujua kama Lucky anatoka kwenye familia ya kitajiri sana huenda kuliko wanafunzi wote chuoni hapo, hakuwa akijionesha kuwa kwao uwezo upo tena mkubwa, alionekana mwanafunzi wa kawaida kuanzia mavazi, misuko ya nywele na vitu alivyokuwa anatumia.
Familia yake yote ilikuwa ikiishi pembezoni mwa jiji la Dar es salam msasani karibu kabisa na bahari ya hindi, Mama yake aliyejulikana kwa jina la Jenipha alikuwa mganga mkuu katika Hospitali ya Muhimbili, kaka yake anayemfata alikuwa mmiliki wa makampuni matatu ya usafirishaji madini kwenda nje, huku baba yake mzee Edward akiwa mfanyabiashara mkubwa wa kimataifa aliyekuwa na jina kubwa mno Africa mashariki ya kati.
Utajiri wa familia yake ulikuwa mkubwa kuliko hata wa viongozi waliokuwa madarakani. Iliishi kwa upendo muda wote, majirani waliiangalia kwa jicho la tatu namna inavyoishi hiyo familia, waliyatamani maisha yao wanayooneshana wakiwa nje, kitu kilichokuwa tofauti kwa mama mwenye nyumba Jenipha aliyekuwa anaiona bora jana kuliko leo, ila haikuonekana hivyo kwa majirani kwa sababu waswahili walishasema " usilolijua ni sawa na usiku wa kiza"
Maisha ya chuo kwa Lucky yalisonga mbele, Mariam, Tunu na Amina waliamua kumuacha kama alivyo, wao wakaendelea na ya kwao, walimtoa thamani na kumuona mjinga asiyejua kitu na huenda ametoka shamba ( kijijini) ndio maana anakuwa hachangamki, ila lililokuwa moyoni mwake hakuna aliyeweza kulifahamu kwa haraka, na alikubali kuonekana mjinga mbele ya wanaojiona wajanja ili maisha yake yaweze kusonga mbele..
"Rafiki yangu namuonea huruma sana huyu mwenzetu, yani anaishi kama mtu wa kijijini mshamba mshamba kimandazi mandazi hivi tu sijui yukoojee, yani ni kajitu tu kapo kapo sio hata kajanja kananiboa kama nini msiiiiu"
Asubuhi ya Jumatatu moja Lucky akiwa bafuni anakoga kujiandaa kuingia kwenye kipindi ambapo wao walishajiandaa, Tunu alisema na wenzake namna anavyomchukulia Lucky kwa kipindi hicho mbali na nyuma alivyokuwa akimueshimu.
"Si bora mandazi hayachachi? Ila achana naye mshamba tu huyo shoga yangu, ukimuita haitiki, ukimsemesha anajibu shoti, ukimuomba hiki mpaka atake, ana nini kwani hadi tumbembeleze bhana, uzuri wa kutuzidi hana, akituzidi sehemu nyingine tu lakini sio sura, na shepu pia tumepewa ana nini cha mno? Akwendege uko tufanye yetu tumpotezee aishi kivyake" Alidakia Amina.
"Mimi nilidhani mnanikalisha chini kusema vitu vya maana kumbe ni huyu tahira, achaneni naye bhana. Kila mmoja mzuri humu ndani hana cha kuringia na kila mtu nyodo anaziweza, ametunyodoa tumnyodoe basi kila mmoja ashike hamsini zake, tena sasa hivi niwa kupewa visa mpaka chumba akihame hiki asilete mambo meusi. Twendeni darasani tusije kukuta professa ashaingia yakawa mengine kisa kumuongelea huyu taka taka" Alidakia Mariam.
"hhhhhmmmmm!" Aliguna tunu. " kumbe na wewe umo?"
Walinyanyuka na kicheko kila mmoja akabeba mkoba wake na kwenda darasani. Lucky alitoka bafuni akiwa na khanga moja mwilini akakaa kitandani na kujifuta futa maji bila ya kujali kama kile kilichoongelewa dhidi yake amekisikia au laa, hakukaa dakika akanyanyuka na kusogea kwenye kioo kujiangalia mwili wake wote ulivyo. Alivuta mafuta aina ya lotion akajipaka baadhi ya sehemu za mwili wake, alipomaliza aliitoa khanga mwili ukabaki tupu kisha akavaa nguo za ndani zilizokuwa kwenye henga.
Alimaliza kwa nguo za chuo akabeba mkoba na kutoka ndani, hadi anafika darasani hakuna aliyeweza kumpa habari ya hellow! kwa sababu ya kusikojulikana sana na watu, kwa alivyokuwa anajiweka hakuna aliyeweza kumzoea kwani hata mbinu ya kumuingia haikuwepo, wapo wanaume waliojifanya midomo mirefu kutaka kuingiza mistari ya kumtongoza kutokana na uzuri wa mvuto aliokuwa nao kuanzia sura hadi maumbile, lakini walijikuta wanashindwa na kujionea aibu tu namna ambavyo Lucky hakutaka upumbavu.
Masomo yalipoisha wanafunzi waliokuwa wanamaliza vipindi walitoka madarasani akiwemo mwenyewe Lucky, mkoba wake ulikuwa begani bila kuongea na yoyote akashika njia ya kwenda kwenye chumba anachokaa, alisimama ghafla baada ya kusikia sauti ya kiume inamuita nyuma yake, aligeuka akakutana na sura ya mmoja ya wanaume ambao huwa wanamsumbua sana chuoni hapo kumuhitaji kimapenzi. Aliitwa Deniss.
"Samahani Lucky kwa kukusimamisha" Alisema Deniss akimtazama vizuri Lucky usoni baada ya kuwa tayari wamesimama wote wawili.
"Bila samahani"
"Leo tumebahatika kutoka mapema darasani, vipi tunaweza kuwa pamoja mchana kwa ajili ya kupata launch?"
"Hapana haiwezekani"
"Kwanini Lucky?"
"Sina sababu ila wewe jua hivyo, haiwezekani"
"Hivi unajua kuwa wewe Lucky ni msichana mrembo ambaye kila mwanaume hapa chuoni anakumezea mate? Ila sijawahi kukuona ukiwa na mchanganyiko wa mtu yoyote Yule kuanzia wanawake wenzio mpaka wanaume kwa nini? Nimekuwa nikikufatilia muda mwingi natamani kuwa sehemu ya maisha yako. Natamani kukujua zaidi Lucky tafadhali nikubalie tuwe na urafiki wa karibu wenye kuendelea pengine hapo badaye yanaweza kutokea makubwa zaidi baina yangu na wewe. Tafadhali Lucky"
Alifinya sura Lucky alipoona mtu aliyesimama naye anataka kumletea mazoea ya kijinga asiyoyataka kabisa.
"Hiyo ni moja ya sehemu za maisha yangu Deniss, ndio staili yangu niliyopanga kuishi, halafu usiishi kwa kukariri kuwa kila mwanamke aliyepewa uzuri lazima awe na mchanganyiko wa watu, uzuri wangu haumaanishi kila mmoja anayeniita niitike, heshimu mawazo yangu ili uwe salama nakuomba"
"Una maanisha nini?"
"Nakuomba tu usinisumbue, sipendi usumbufu usiokuwa na maana"
"Unataka kuniambia nikikusumbua itakuwa sehemu ya kuhatarisha maisha yangu?"
"Hautakuwa salama kwa asilimia mia moja"
"Nipo tayari Lucky nisiwe salama kwa asilimia mia moja ila naomba tuwe marafiki wa karibu tafadhali"
" Nisamehe"
Ulipita ukimya kidogo ulio ondolewa na Deniss.
"Ok Lucky, mimi nikutakie siku njema ila ningeomba kupata japo namba yako ya simu basi kama hutojali, nadhani nitajiona mwenye bahati sana"
"Samahani Deniss pia haiwezekani kupata namba yangu"
"Dah! Okey poa"
Lucky aligeuka na kuondoka zake huku nyuma akimuachia lawama nzito kijana Deniss namna alivyokuwa anatingisha mauno yake aliyojaaliwa na Mwenye Ezi Mungu, ni kama alikuwa anafanya makusudi, kijana huyo hakuweza kugeuka kirahisi hadi alipoona Lucky ameishilizia ndio aliweza kugeuka na kuanza kutembea mate yakimtoka, moyoni alikuwa na maumivu makali ya kukosa bahati ya kupata walau namba ya Lucky msichana aliyevutiwa naye tokea anajiunga naye siku ya kwanza darasani.
Lucky alifika chumbani kwake akaweka begi kwenye kiti akajitupa kitandani kidogo, alilala chali macho yakawa juu na kuingia katika wingu zito la msongamano wa mawazo, dakika kumi mbele tayari alikuwa anabubujikwa na machozi ambayo hakufahamu yanatokea wapi, yalikuwa ni machozi yaliyozungukwa na maumivu makali kutokana na kumbu kumbu zake za maisha, yaliuteketeza uzuri wote alionao usoni, marafiki zake anao kaa nao waliingia kipindi hicho hicho bila yeye kusikia hata mlango ukifunguliwa, huenda kutokana na kuwa mbali kimawazo, Tunu, Mariam na Amina walisimama vizuri mlangoni kumwangalia kwa makini, walipoteza zaidi ya dakika nzima wakashuhudia jinsi anavyobubujikwa na machozi na anavyoteseka, huruma iliwaingia wakamsikitikia kisha kumsogelea taratibu, Mariam alifika karibu naye akakaa pembeni yake na kumshika pajani, Lucky alisisimka, alishtuka akawaangalia na kuanza kufuta machozi.
"Why Lucky why why, why my dear friend why!" Alisema Mariam kwa uchungu, aliendelea. "Kwanini unatufanya kama watoto lakini, kwa nini unatufanyia vimbwanga vya roho Lucky kwanini, kwanini jamanii! Kitu gani kinakusumbua moyoni mwako hadi sasa? Si utuambie jamani mbona unakuwa hivyo? Unatuchukuliaje sisi? Unahisi sisi ni wanyama hatustahili kushirikishwa katika shida? Unahisi sisi ni watu makatili kiasi icho hatutoweza kukusaidia?" Aliuliza Mariam kwa hasira zilizoambatana na uchungu. Lucky alinyanyuka akakaa, sura yake ilijaa huzuni, ilijaa maumivu, ilijaa kila aina ya mateso ya maisha anayopitia.
"Hamna kitu Mariam" Alisema kwa ufupi akivutia mafua kwa ndani na sura yake kuielekezea chini kama mtu mnyonge asiyekuwa na haki yoyote, akamuweka katika kipindi kigumu cha kumkatili moyo Mariam.
"Dah! mimi ni rafiki yako Lucky, nakuomba usinifanyie hivyo nakupenda, mimi nakupenda Lucky, naumia sana ninapokuona katika hali hii sema kama unaumwa tukupeleke hospitali mbona marafiki zako tunakupenda sana why wewe huoneshi upendo kwetu jamaniii?" Aliongea kwa uchungu Mariam lakini Lucky hakuwa tayari kuongea chochote, Mariam naye alianza kulia baada ya kuona ni kama vituko wanafanyiwa na binti huyo wanayeishi naye chumba kimoja bila ishara ya kuonesha kabisa kuwa nao, Tunu aliingilia kati akamzuia Mariam kulia, walichukuana wote watatu wakatoka nje wakamuacha Lucky peke yake, walipofika nje walisimama na kuanza kushauriana nini wafanye juu ya rafiki yao huyo japo walishaamua kumtoa thamani ikiwa yeye haoneshi ushirikiano nao, ila hali waliyomkuta nayo ilibidi wabadili mawazo yao na kutafuta mbinu ya kumsaidia kumwondoa katika janga alilonalo.
"Kiukweli hali ya Lucky mimi inanichanganya sana siwachifi, yani bora kuishi na nyoka ikawa inakudonyoa tu huenda maumivu yataisha kuliko kuishi na mtu wa aina hii Akyamungu" Alisema Mariam.
"Mariam unajiumiza kichwa tu my dear friend, hadi machozi yanakutoka kabisa kwa mtu kama huyo?" Alihoji Amina.
"Sijafundishwa hivyo Amina, roho yangu ni nyepesi sana ninapomuona mtu anateseka kwa kitu kisichojulikana"
"Mimi nina wasiwasi Lucky ametokea kwenye maisha ya shida sana ndio maana yupo vile, au hapa mjini ni mgeni maana kila kitu hajiwezi, story hawezi, kampani hakuna, kicheko kwake hakijawai kuonekana, kuongea na mwanaume hapana, kuvaa hajui anavaa tu visasampure vya ovyo ovyo hajui kudamshi jamani! Yani ni kajitu kapo kapo tuuuu sijui hata! Sasa sisi tumchukuliaje? Ujue anazingua sana huyu demu e au mwangaa!?" Alisema Tunu akashika kiuno.
"Yani Tunu wewe acha tu anazingua zaidi ya sana halafu umegusia pointi nzuri, anaweza kuwa mwanga kweli waswahili wanasema muogope mtu mkimya, isije kuwa anatutoa ujungu usiku maana kuna siku huwa naota ndoto sizielewi elewi, ila nina wazo" Alisema Amina.
"Wazo gani? Aliuliza Mariam.
"Twende tukapeleke malalamiko kwa msimamizi, kiongozi. Tusikae nalo hili jambo yakaja kutokea makubwa zaidi ikawa shida, twende kwa kiongozi tumueleze moja mbili tatu nne, kama ni mwanga siku akitugeuza misukule tukawa hatuonekani ghafla hapa chuoni wajue ni yeye"
"Yani leo umeongea kitu kizuri wewe mshenzi, aidia nzuri sana hiyo, twende huko huko tumueleze kuwa mwenzetu hatumuelewi kabisaaaa tumpe A to Z" Alisema Tunu.
Wazo hilo lilipita kwa wote wakatoka taratibu hadi sehemu alipokuwa msimamizi wa wanafunzi wote chuoni hapo, alikuwa mwanadada aitwaye Sophia wakakaa chini na kuanza kumpa moja mbili tatu kuhusu Lucky, Lucky mwenyewe hakuwa anajua chochote wanachofanya watu anaoishi nao chumbani, alijipozea tu kitandani wimbi la mawazo likizidi kumtafuna.
"Dada Sophia tumeishi na mwenzetu Lucky mwaka sasa, lakini kwake hatujawai kuona kicheko, tabasam, furaha zaidi ya huzuni, kilio kisichoisha na ukimya basi, tunahisi atakuwa ana kitu kikubwa sana akilini mwake kinachompelekea kuwa hivyo. Ila sasa hali yake inatutesa, kama kuna uwezekano mhamisheni hata chumba chengine au kaa naye chini umsomeshe umpike akueleze kinachomsumbua, abadilike sisi hatuwezi kuwa na mtu wa aina ile, wewe mtu hatujui kicheko chake, tabasam kwake ni kama sikukuu, aka! sisi hatuwezi dada Sophia, pia tunamuonea huruma maana si usiku si mchana yeye kilio, kilio na yeye ndio nini sasa?" Alisema Amina akitumia zaidi ya dakika tatu kuongea, kila kitu kilichokuwa kinaendelea kwa dada Lucky alikiropoka mbele ya Sophia ili kuangalia kama uwezekano wa kutatua tatizo lake utakuwepo au laa.
"Mmekaa naye mwaka sasa katika hali hiyo, kwa nini hamkufanya hivyo kipindi cha nyuma mfanye sasa?" Aliuliza Sophia baada ya kumsikiliza Amina kwa makini.
"Sasa sisi tulikuwa tukimuangalia tu labda atabadilika lakini wapi habadiliki, imefikia sehemu tumehisi kama hajaharibika kisaikolojia basi ni mwanga" Alisema Amina.
"Mmejaribu kumkalisha chini kumweleza?"
"Ndio tena sii mara moja wala mara mbili"
"Okey sawa nimewasikia nitalifanyia kazi"
"Tena ukikaa naye mwambie kabisa tumechoka, tumechoka tumechoka tumechoka, wewe jitu halijui hata kucheka bhana" Alidakia Tunu akaongea kwa hasira.
"Sawa nimewaelewa rudini chumbani kwenu" Alisema Sophia kwa muonekano wa kuwa mkali kidogo, ila hawakushtuka ilikuwa kawaida yake, waliinuka kurudi chumbani kwao kabla ya kufika popote Tunu aligeuka.
"Halafu bora umwite sasa hivi uongee naye maana yupo analia huko chumbani, kinachomliza hatukijui"
"Naomba mrudi kwenye chumba chenu tafadhali"
"Tunarudi ndio ila uliambie! Tumeshachoka. Hatuendani naye hata kidogo yani"
"Rudini chumbani kwenu" Alikuwa mkali Sophia akasimama.
Hawakumsemesha jengine walitoka wakatembea hatua kadhaa ambazo ziliwafikisha mlangoni wakafungua na kwenda moja kwa moja chumbani, Lucky tayari alikuwa ashamaliza kulia muda huo alikuwa amekaa kitandani anajisomea, pia hawakushangaa kwani ilikuwa moja ya kawaida zake, walipita kila mmoja akapanda kitandani kwake wakatoa simu zao na laptop kwa ajili ya kuanza kuchart na kuperuzi katika mitandao mbali mbali.
Lucky aliwaangalia akatingisha kichwa na kuendelea kujisomea huku wao wakiwa wanachart, masaa yalisonga mbele siku ikaisha na kuingia siku nyingine, ilikuwa jumamosi kulikuwa hakuna anayeingia darasani, kila mmoja alichelewa kuamka isipokuwa Lucky alieamka saa moja na kuingia katika dimbwi zito la mawazo, mlango uligongwa akashtuka na kujiuliza nani anawagongea mlango asubuhi yote hiyo wakati dada wa usafi huwa anaingia saa mbili na nusu. Uligongwa tena akaweka khanga yake vizuri aliyokuwa ameiegesha tu mwilini kisha kuinuka kitandani, alisogea hadi mlangoni akafungua na kuchungulia nani anagonga, macho yake yaligongana na macho ya Sophia kiongozi wa chuoni hapo, woga ulimuingia mapigo ya moyo yakaamka akamkaribisha huku moyoni akijiuliza mbona Sophia yupo hapo kwa muda huo.
"Karibu Sophia"
"Asante nishakaribia mambo?" Alisema Sophia baada ya kukaribishwa.
"Poa."
"Nimekuharibia usingizi wako ee? Nisamehe mwaya"
"Wala! Nilishaamka zamani usijali kuhusu hilo"
"Mapema yote hii?"
"Yeah kuna masomo jana yalinichanganya kidogo ndio nilikuwa nayapitia, si unajua asubuhi kunakuwa hakujachanganya hivyo masomo yanaingia?"
"Ni kweli nalijua hilo, na wenzio vipi hao tayari au bado wameuchapa?" Aliongea akiachia tabasam.
"Wao bado wamelala"
"Okey poa, basi tafadhali nakuomba ofisini kwangu mara moja nina maongezi na wewe, samahani sana lakini" Alisema Sophia, Lucky akashangaa na kupokea mshtuko mwilini mwake.
.........
Muendelezo sh 1000
Njoo WhatsApp 0743433005.