NAKUPENDA BILA MIPAKA: 109 - 120 SEASON THREE
109
Mwenzenu nimechambwaaa, nishanangwa siamini kama ndiyi nilifunguliwa mlango mimi, nikapelekwa mtoko mimi, na nikawa natumiwa ujumbe. Leo hii kwa ukali nafokewa macho yametoka mpaka natetemeka. Nilikuwa nimechoka sana.
Sijui nini kiliendelea, sijui, lakini nilipo amka nilikuwa hospitali. Nilikuwa pale nimechoka sana. Hata mara baada ya kuamka machozi ndiyo yalikuwa yananitoka. Maneno pekee niliyokuwa nakumbuka kwenye kichwa changu ni yale maneno makali ya kuumiza na kuvunja moyo wangu vipande vipande. Roho yangu ilikuwa inauma sana.
Kila nilipoyafumba macho yangu machozi yalizidi kunimwagika. Nilikumbuka ile sauti ya ukali ya Mr Gallen akifoka “unadhani wewe ni nani?, unafikiri wewe ni nani kwenye hii nyumba. Am asking who do you think you are. Unafikiri unaweza kufanya chochote unajisikia kwa mama yangu.
Upo hapa kumuhudumia ili nikulipe, sio kumuua mama yangu. Upo hapa kufanya kazi kwaajili yake sio kumpa maumivu. Wewe unajiona nani, ni malaika wewe, ni Mungu wewe eemh you are so stupid, stupid. Omba sana mama yangu apone omba sana. Otherwise.”
Daaaaah!!, nilitokwa machozi huku natazama huku na kule, sioni hata ninayemfahamu hapa. Nipo peke yangu, ilikuwa ni usiku na sijui ni saa ngapi. Hata nilimbuka maneno ya kaka yangu Baraka aliyokutana nayo, sikumbuki mengi lakini nilikuwa nakumbuka vile alivyokuwa anasema alimwambia Mungu wake ya kuwa Mungu wa Mbinguni Amkumbuke, amtoe kwenye vifungo.
Nilikaa pale kitandani, ninajishangaa tu, machozi yananitoka nalia. Asikwambie mtu jamani, kuna maumivu halafu kuna haya ya kichambo cha mtu ambaye unampenda na ulianza kuonekana kuna upenyo. Tena mbele ya mtu ambaye anajifanya kumpenda sana. Naona kama nimevuliwa nguo, nililia ule usiku. Eti upo hapa ufanye kazi nikulipe, ni kama tu anasema maskini wewe una nini. Niliona kama Mungu amenisahau mimi jamani.
NAKUPENDA BILA MIPAKA:110
Hapo nawaza mtoto wangu, nawaza simu yangu nimeacha mama na ndugu zangu watakuwa wananitafuta sana. Nilikuwa nachanganyikiwa mimi. Nilikaa pale kitandani nakumbuka sana huku nalia, huku nalia nilikumbuka kuwa niliambiwa nikae na Mungu.
Unajua mimi sikuwa nataka kumuumiza mama, mama yeye mwenyewe kwa upendo wake alitaka kuwa karibu na mimi, tukasaidiana na Maria, na alikuwa amefurahi. Kilichotokea ni ajali, inaweza kutokea popote, lakini saivi naambiwa nataka kumuua.
Mazuri yote nimefanya kwa mama sasa hivi hakuna hata moja linakumbukwa, shetani akitaka kuharibu jambo lako huwezi kuelewa. Mimi huyo, nikakumbuka mengi niliyowahi sikia kuhusu Mungu wangu.
Unawez kucheka hapa nilikumbuka hata Movie ya Yesu vile alifunga na kwenda na wanafunzi wake mlimani kuomba.Vile anaomba uso wake ukang’ara kama jua na mavazi yake yakawa meupe sana.Nilitamani ghafla kuwa kama vile.
Nililia nikisema kwa uchungu “Yesu nipe kibali chako, nipe kibali cha kuonekana, Nipe kibali cha kukubalika, nipe kibali cha kuwa wako, nipe kibali kwenye kila kitu changu cha maisha.
Nipe Kibali kazini, nipe kibali kwa marafiki, nipe kibali kwenye mahusiano, nipe kibali hata kwenye malezi na kila ninapotembea naomba kibali chako.
Natamani kung’ara kama uso wako ulivyong’ara pale mlimani ukiwa na wanafunzi wako, watu wakiniona waone napendeza na mavazi mazuri ning’are kila kona ya maisha yangu kuanzia muonekano wangu, sura yangu na kila kitu changu. Mungu nisaidie, nimechoka, nimechoka sana.”
Kadri nilivyokuwa nalia hapa ndiyo nilikuwa nazidi kuchoka, nilichoka nikalala tena. Bila shaka ni dawa. Nilikuja kuamka asubuhi sasa ndiyo nakutana na dokta, sio dokta yule hapa ni wa hii hospitali hapa. Alitabasamu na kusema “Pole sana, unajisikiaje?”
Nilimtazama na kusema “naendelea vizuri sana.”
NAKUPENDA BILA MIPAKA:111
Alitabasamu, nikamuuliza “tatizo nini, na nipo hapa kwa muda gani?”
Huyi dokta aliniambia “usijali mshtuko tu kidogo, na unaendelea vizuri.”
Nikamtazama na kusema “naweza kuondoka leo?”
Alinitazama na kusema “unaweza ila sio sasa.”
Nilimtazama na kusema “ndugu zangu watakuwa wananitafuta, unaweza nisaidia simu.”
Alinitazama na kisha alinipatia. Nakumbuka namba ya kwanza alikuwa ni mama yangu. Mama alipokea nikaita “mama!!”
Mama alisema “mwanangu, mwanangu upo salama?”
Nilivuta pumzi na kusema “nisamehe mama kwa kuwatia wasiwasi, jana nilipata changamoto kazini nikaanguka na kupoteza fahamu. Wakanileta hospitali, ndiyo nipo hapa na naweza ruhusiwa leo.”
Mama alisema “ni wapi nataka kuja.”
Nikamuuliza dokta maana sijui hata nipo wapi. Dokta alinitajia ni hospitali ya kulipia kubwa sana hapa mjini. Mama akasema “mwanangu ndiyo ipo wapi sasa?”
Nilishusha pumzi na kumwambia mama aingie chumbani, achukue pesa kisha atafute tu pikipiki aje bila hivyo sio rahisi. Mama alikubaliana na mimi.
Wakati namshukuru Dokta narudisha simu aliingia dada Maria akiwa hana raha. Aliponiona alisema kwa upole “nesi, unaendeleaje?”
NAKUPENDA BILA MIPAKA:112
Nilimtazama machozi yakanitoka nikisema “natamani nirudishe siku nyuma nisimsikilize mama na kumtoa. Ulisikia amesema nataka kumuua mama yake, hivi dada Maria kweli baada ya yote nnayofanya, ninavyompenda mama kama mama yangu mzazi nawezaje kufanya hivyo mimi. Nimejisikia vibaya sana.”
Dada Maria alisema “naomba usilie mdogo wangu, naomba usilie na unajua Boss ana hasira tu, hajamaanisha. Hujui tu ana wasiwasi sana kila muda ana kuulizia. Yule Dokta anajiongelesha na kujifanya ndiyo mwema sana lakini Boss kila muda anakuulizia na kujilaumu. Hajalala, usiku wote yupo hapa hospitali.”
Mimi tena nilisema “yupo hapa kwaajili ya mama yale sio mimi. Binadamu tunasahau haraka sana ila Mungu amsaidie mama. Atapona na yeye ndiyo anaweza kunitetea mimi maana sikumtoa kwa kutaka.”
Dada Maria alinitazama na kusema “mama ameamka asubuhi hii, anakuulizia wewe.”
Nilimtazama na kusema “waoooo!!, afadhali ameamka, nilikuwa naogopa kama angekufa ningeishia jela mimi. Asante Mungu, nakushukuru Mungu. Dada Maria naweza pata mkoba wangu tafadhali.”
Alinitazama na kusema “wacha niagize dereva anavyokuja aje nao.”
Wakati huo namuona Mr Gallen mlangoni ndiyo anaingia, amechoka, uso wa upole. Mimi tena nimenuna hapo sicheki, yeye si ameanzisha mimi ndiyo namaliza sasa. Ameyataka yeye mwenyewe kunichokoza binti wa watu sasa wacha aone nilivyo. Alimtazama Maria na kusema “naomba kuongea na Nazwi.”
NAKUPENDA BILA MIPAKA:113
Mimi nimelala tu kichwa kwingine. Aliniita kwa Upole “Nazwi!!”
Niligeuza kichwa na kumtazama, halafu nilishusha pumzi nikasema “Boss nisamehe sana kwa kuvuka mipaka.
Nisamehe kwa kila nilichofanya, nilifanya na nikavuka mipaka. Sitarudia tena, najua na natambua mimi ni mfanyakazi ninayesubiri kulipwa na wewe na sio vinginevyo. Chochote nilichofanya ni kukiuka sheria za kazi na nipo tayari kuwajibishwa.
Sina nia ya kumuua mama yako, najua ni mfanyakazi wake. Sio mama yangu yule, ninaye mama yangu pia. Nisamehe sana nilizidisha, nisamehe.”
Najilalamisha kupitia maneno yake nikajikuta nimeanza kulia. Unajua maneno yake yalikuwa yananikera sana. Natamani ungeona alivyokuwa anafoka mpaka anatetemeka jasho linamtoka. Niliumia sana. Niliumia. Na yeye maneno yangu yalimuumiza.
Nilisikia akisema “usifanye hivyo tafadhali, usiseme hivyo Nazwi. Sijui hata kwanini niliongea maneno yote yale. Maria amenielezea kila kitu.
Hata bila Maria nilitakiwa nikuamini kwasababu unampenda mama, ni mama yako pia ninyi ni marafiki.
Sijui kwanini sikufikiria hata nikakubali hasira initawale. Nazwi naomba nisamehe sana, Nakuomba na nina maanisha hili.”
Nilinyamaza, huku moyoni naona raha anaomba msamaha lakini bado nina maumivu na yale maneno. Mimi kwenye maisha yangu bora mtu achukue fimbo anichape, ila sio kufokewa tena na maneno makali yenye dharau.
Aliniita tena na kusema “Nazwi, utasahau na kusamehe, nakuomba, nakuomba nisamehe sana.”
Nilishusha pumzi na kusema “usijali Mr Gallen, nimekusamehe. Unaweza kuniacha peke yangu sasa nahitaji kupumzika.”
Eenh mimi huyo namwambia hivyo Boss wangu, sasa Je, si naumwa sasa atabishana na mgonjwa, hawezi, hawezi bishana na mgonjwa na mimi wacha nitumie nafasi tajiri huyu nitamsimangia wapi mimi.
NAKUPENDA BILA MIPAKA:114
Kwa upole alinitazama akaniuliza “unajisikiaje sasa hivi?, unaumia popote, unataka kula nini?”
Nyie huyu muanko mnaelewa sijui, amechanganyikiwa, ananitazama kwa huruma kama alie. Mimi tena nipo “usijali, mama atakuwa hapa watanihudumia. Nenda ukaendelee na mama.”
Mimi mimi mimi jamani, kakiburi ka madeko kwa Muanko kametokea wapi, na yeye ananiambia “please usiseme hivyo, najua unaumia na maneno yangu. Lakini tafadhali nakuomba sana.”
Nilimwambia kwa upole “Boss hapana sina hasira, mimi ni mfanyakazi wako nakuheshimu sana. Najisikia vibaya tu kwasasa, usijali tutaongea wakati mwingine.”
Alinitazama na kusema “nipo nje ukihitaji chochote nipo kwaajili yako Nazwi, am here for you. Mama yako ameamka na amekuulizia.”
Nilitabasamu na kusema “nimefurahi kwaajili yake, nashukuru Mungu yupo hai.”
Alinitazama hata alifuta machozi yake, mimi nashangaa analia jamani, analia kwaajili yangu, analia ameniumiza mbona makubwa haya. Wakati anajiweka sawa mimi hapo nipo kimya mama yangu ni wazi aliwasiliana na dokta nikaona huyo akiwa na Dee na Baraka.
Nikafurahi kuwaona, mama alifika kunikumbatia, ila Mr Gallen hakuwa sawa akawa anatoka. Sasa Dee akawa ananiminya. Na mimi namminya ni mbea huyu hajali hata mgonjwa. Mama akauliza pale ilikuwaje, nikaelezea.
Kubwa zaidi kaka yangu amependeza na amekuwa mpole sana. Aliniambia kwa upole “Mungu atakuponya dada pole sana.”
Nilisema kwa upole “nashukuru sana, mama fanya unavyo fanya tuondoke wote
Mimi naendelea vizuri.”
Mama alisema “ni sawa mwanangu kama upo salama.”
NAKUPENDA BILA MIPAKA:115
Wakati huo na Maria akawa anaingia, basi nilimkaribisha na kumtambulisha kwa ndugu zangu na yeye pia nikawaambia ndugu zangu kuwa ni ndugu wa ninapofanya kazi. Dada Maria alisema “hongera sana mama una binti mzuri sana. Tunampenda.”
Nilicheka tu na kufurahia.
Mama akasema “wacha nikafuatilie basi mwanangu.”
Nilitabasamu nikisema “sawa mama.”
Kaka alisema “wacha nikakusaidie mama.”
Nilitabasamu, nikamuuliza “dada huendi?”
Hapo nawasha simu yangu.Dada Dorice akili hata hana, alisema “naendaje hapa nataka kujua yule ni Muanko, na kama ndiye mimi mwenyewe ningekuwa kama Dokta. Mbona anavutia hivyo kama kijana sio kijana, muanko hapo sio Muanko, muzee sio muzee, mubabu sio mubabu. “
Nilimtazama na kusema “rafiki yangu hivi unajua naumwa na wala sitaki kucheka.”
Alicheka akisema “baba mzuri huyu jamani sasa wakati kijana mdogo mdogo alikuwaje?.”
Nilimtazama na kusema “hutoniuliza nini kilitokea?”
Akanitazama na kusema “nilisahau, eenh niambie shida nini. Tumehangaika mpaka kazini nimekimbia leo.”
Nilivuta pumzi na kuanza msimulia.
Dorice alisikitika akisema “hawa matajiri sijui hata huwa wanatuonaje. Lakini potezea rafiki yangu.
Mimi je huko kazini kila siku kama mtoto, ndiyo maisha ya kuajiriwa wanahisi wana miliki mpaka roho zetu. Muhimu mama yao ameamka.
Kama namuona huyo dokta sasa, itakuwa anajiona yeye ndiyo yeye.
NAKUPENDA BILA MIPAKA:116
Unataka kunambia na Muanko umemkatia tamaa shooo kisa kafoka?”
Nilimtazama na kusema “upo upande wangu au wamuanko chagua team mapema.”
Alicheka akisema “nakuachaje shoga yangu.”
Shetani hatajwi, dokta wangu sasa cha maringo kaingia. Alivyo kapendeza sasa. Alisalimiana na Dorice akaniuliza “nesi wangu unaendeleaje?”
Nilitabasamu na kusema “Mungu mwema, naweza kwenda nyumbani sasa.”
Alitabasamu na kusema “jitahidi upumzike ndiyo utaendelea na kazi unahitaji mapumziko.”
Nilitabasamu, maana najua kwake hii ni fursa awe na muanko vizuri. Basi akasema “mimi nilikuwa nakujulia hali, ninaenda kwa mama sasa tutawasiliana.”
Aliondoka, nikasema “ndiyo cha maringo wetu huyo.”
Akasema sasa dada Dee “ingawa ni mchawi karaba ni mzuri shooooo, mzuri haswa.”
Nilimkata jicho, akasema “leo kazi ipo.”
Nikatabasamu tu.
Familia yangu ilifanya vile vya muhimu tu maana kila kitu kililipwa na Boss wangu. Kusema ukweli wa moyo nilikuwa bado nina maumivu sana hivyo sikutaka kabisa kukutana na Boss wangu. Mimi na ndugu zangu tuliondoka pale hospitali.
Zaidi ya dokta aliyekuwa ananihudumia. Sikumuaga Maria wala Mr Gallen, sikutaka hata jisumbua nikamuone mama. Maana yale maneno, kule kufokewa acha tu ninavyojisikia.
Fikiria wewe huyo unayempenda, unamuhangaikia kama ninavyofanya kwa mama yake zaidi hata ya ujuzi na upendo wa kazi ua uuguzi nafanya zaidi. Ni kweli sitegemei kulipwa maana napokea mshahara lakini ule utu.
NAKUPENDA BILA MIPAKA:117
Maneno yamemtoka Boss kama vile hanijui na wakati tulianza elewana. Hii iliniuma sana moyo wangu. Nilijisikia maumivu makali na siwezi kusema ma mtu nipo tu mimi ndiyo najua nilivyokuwa ninajisikia.
Hakuna kitu kizuri kama kupenda, kumpenda mtu, kumuwaza na kumfikiria yeye. Lakini omba sana usikosee kupenda, ukikosea kupenda hisia hugeuka Utumwa.
Mimi hapa, nimekuwa mtumwa wa hisia zangu mimi mwenyewe. Ninampenda sana huyu mtu lakini naona kabisa mimi sio wa aina yake, na sina thamani mbele yake na sitapata kile nataka kwake ndiyo maana ananifanya vile anataka yeye.
Moyo wangu unaniambia Nazwi umetoka kwenye maumivu.Hapa utaumia zaidi na zaidi, acha mama, acha kabisa kaa mbali naye, sahau kuhusu yeye hata hivyo ni mkubwa kwako. Utapata wako tulia. Moyo huo sasa unanipa zake ushauri sijui hata kama naelewa. Hapo tupo kwa gari nimetulia zangu kimya safari ni nyumbani.
Tulifika mpaka maeneo jirani na nyumbani, Mr Gallen akatuma Ujumbe. Huwezi kuamini, huyu baba cha kununa,
Ni mimi ambaye nilikuwa namuona ndiyo natuma natabasamu, sasa hivi ni yeye sasa ndiyo anatuma ujumbe yaani ni hivi yeye ndiyo ananibembeleza tena na hili darasa mama yake ndiye alinifundisha.
Weka ugumu muone, mwanamke ringa, sio kila muda unapatikana tu kwaajili yake, usipige kelele muoneshe msimamo wako.Ndiyo nipo sasa naonesha ugumu mimi.
NAKUPENDA BILA MIPAKA:118
Sasa hapo mimi ndiyo najiambia “Mr Gallen mbona bado, utalipia ulichonifanyia, safari hii utajifunza kuwa hata maskini wana msimamo tena sio msimamo wa kitoto. Mbona bado muanko, wewe si ulikuwa unajifanya kufoka mpaka unatetemeka. Eenh nacheka kimoyomoyo.
Unajua ameniandikiaje “Nazwi, What are you doing, umeondoka hujaaga kweli?. Unakosea, usifanye hivyo.”
Yaani huyu si ndiyo alikuwa anajiona yeye ni chakununa kila dakika, anapiga simu hata sipokei, mimi naitazama tu.
Mwisho wa siku nikaona ananisumbua nakuambia muanko huko alipo kachanganyikiwa anapiga simu, anapiga simu kama sio msomi. Kama nicheke vile ila hasira mtoto wa kike mimi zimenikaba.
Tulifika nyumbani, baada ya hapo ndugu zangu walikuwa wananihangaikia. Zaidi ya yote nilifurahi sana kumuona binti yangu Priya. Alinipokea kwa furaha yeye hajui hata kama mwenzake naumwa ugonjwa kichambo.
Ni kunidandia hivi na vile na kunidai zawadi hata mimi yake alisema “Priya unataka kuniulia binti yangu sasa, haya njoo chukua hela ukanunue pipi halafu ucheze hapo nje umenisikia eeh!!!”
Tulijikuta tunacheka kidogo, Dorice alihakikisha naoga na nikabadili nguo sasa hata mwili naona mwepesi kiasi chake. Mama na yeye alinipatia supu alichemsha basi nikanywa pale, nikawa nahisi kuchoka sana. Mama alinitazama akisema “kunywa maji mwanangu, maji mengi ya kutosha eenh.”
NAKUPENDA BILA MIPAKA:119
Nilimtazama mama yangu, alinipatia maji nami nikanywa halafu nikajilaza, na Dorice alilala pembeni yangu. Mama alisema “sasa hapo mtalala mpaka, Dorice muangalie ndugu yako.”
Aliitikia tu “sawa mama.”
Nililala, lakini naomba niseme kitu kimoja, jamani au nayakuza, mimi usikute nayakuza. Maumivu hayaniachi mpaka kitandani.
Tena ndiyo nakumbuka hata dokta Kabale sasa alivyokuwa anasema “Relax acha na huyo, mara aseme nilikuonya hukunisikia, unanisikitisha sana.”
Dokta ananiambia mimi nasikitisha kweli, huku unasikia kwa ile sauti nilikuwa nasema nzuri yoooh amekasirika sasa naona kama nini sijui sauti ya kutisha “who are you, unajifanya unajua sana, unataka kuonekana wewe ndiyo wewe humu ndani, wewe sio chochote ni unafanya kazi ulipwe.”
Acha tu nalala huku machozi yananitoka, kiasi Dorice alinikumbatia akisema “Nazwi stop this. Umetoka hospitali unataka kurudi tena. Najua unaumia, najua unapitia wakati mgumu tafadhali acha yapite tu, yaache.”
Nililia nikisema “najisikia vibaya sana, naumia sana kipenzi.”
Dorice aliniambia “sahau haya, Ipo siku Mungu atatusaidia tu. Acha tafadhali.”
Alianza kunibembeleza hata nikalala.
Nililala sana, nililala mpaka mida ya jioni hivi. Sasa nilikuwa nikiwa nimelala nasikia kama mtu analia hivi, ilinibidi niamke, nilipoamka niligundua kuwa nilikuwa sahihi. Ni kweli Dorice alikuwa analia, alikuwa analia tena kilio cha maumivu makali sana.
Makala nyingine zinazocheza na ladha yako
Mapendekezo haya yanatokana na kile unachosoma sasa + Endelea kugundua zaidi


Maoni