DO YOU LOVE ME.... 02 (S2)
ACT LIKE A WITCH
Asubuhi iliyofuata niliungana na Rely kumsaidia kumtafuta Mama yake kila kona. Tulizunguka maeneo mengi ya Zanzibar bila hata mafanikio yoyote. Wapi amekwenda? Ndio lilikuwa swali linaloumiza ambalo lilituchosha sana.
Basi, tulipitia hospital ambako tulimkuta Baba Rely (Mr Taz) akiwa kitandani akipatiwa matibabu. Ule mwili wake wa kutisha kama jumba, sura yake yenye mashavu mazito na makubwa pamoja na mng'ao wake, vyote vilipotea.
Mr Taz alionekana kama Kijana wa makamo ambaye ameathirika na matumizi ya madawa ya kulevya. Alikonda na kupoteza mvuto. Rely alimsimulia Baba yake kuhusu kupona kwa Rola.
"Namuomba Rola, aje hapa nimuombe msamaha. Siku zangu za kuishi zinahesabika. Najutia kwa niliyoyafanya" Mr Taz alizungumza kwa sauti iliyotapakaa maumivu.
"Baba, Rola amekuwa mkali hata sisi wenyewe anatuchukia"
"Nataka kumuomba msamaha, tafadhari namuomba hapa" Alisistiza Baba Rely.
Hatukuwa na namna nyingine zaidi ya kurudi nyumbani kwa ajili ya kumwambia Rola kile ambacho tumeambiwa. Kwa bahati mbaya, Rola hakutumkuta.
"Kaondoka, sijui kasema anakwenda kwa Hussein hata sielewi" Thelesia alitueleza.
"Mungu wangu, inamaana kweli Rola ametaka kuingia katika mahusiano na Hussein? Hivi anamjua vizuri huyu mtu? Hussein anasifika kwa utapeli. Huko bara kahama kwa sababu ana kesi ya kutapeli mtu gari. Leo hii yeye anampenda Hussein kweli? Ngoja aje" Rely alifoka kwa hasira sana kisha huyo aliondoka zake.
Nikabaki kuwa mtazamaji tu maana sikujua mengi sana kuhusu huyo Hussein ambaye alikuwa anazungumziwa. Nani wa kumuuliza Hussein ni nani? Ameingiaje katika maisha ya hii familia? Hilo nilikosa, macho yangu yakawa tayari kula kinachoendelea huku masikio yakitamani kusikia mambo kadhaa kutoka pande zote za watu hawa.
Majira ya saa tatu usiku, nikiwa chumbani nilisikia mlio wa honi ukitokea nje kabisa. Nikajua hakukuwa na mwingine ambaye angepiga honi ile isipokuwa ni Rola. Haraka sana niliwahi getini.
Ni kweli nilikuta Rola akiteremshwa katika gari na mwanaume ambaye alikuwa mbavu kiasi. Alinizidi kimuonekano huku akiwa na ndevu za alshababi.
"Huyu ni mfanyakazi wangu, anaitwa Rahim na ni mpenzi pia wa Rely" Rola alinitambulisha kwa yule mwanaume kidharau sana, akiendelea "Rahim, huyu ndio mwanaume wa ndoto zangu anaitwa Hussein. Huyu ndio barafu wa moyo wangu na mwanaume ambaye Baba yangu alinitaka niolewe naye tangu nikiwa mtoto mdogo"
Nilimtazama Hussein kwa jicho la hasira sana, nikamtazama Rola hukj nikitetemeka kuanzia nywele hadi kucha. Meno yangu niliyang'ata kwa hasira. Sikutegemea kitu kama hichi wala sikutegemea kama ningekuja kuoneshewa dharau kwa kuitwa mfanyakazi katika ile nyumba.
Moyo wangu ukapasuka kwa hasira, ndita zikatuhama katika paji la uso kwa muda mrefu sana huku nikifikiria kisha nilisema.
"Rola unanitambulisha mimi kama mfanyakazi wa ndani?"
"Khe! Sasa ulitaka nikutambulishaje Rahim? Ok, niko na mpenzi wangu huyu hapa. Ebu niambie, nikutambulishe vipi? Basi ni shemeji wa yule mtoto wa mchawi. Eenh! Ni mume wa mchawi au sio hivyo?" Rola aliuliza kwa kebei akiwa anachezea ndevu za Hussein
"Mimi ambaye nimepambana na wewe hadi unakuwa mzima, unapona na kuiona dunia ikiwa tamu ndio unanitambulisha hivi? Yapo wapi mapenzi yangu kwako Rola? Zipi ni fadhila za kukusaidia?"
"Kwani kutoa msaada ndiko kupendwa? Unataka nikupende wakati nina mtu wangu? Rahim, mimi kukupa nafasi ya kuishi hapa kama mtu wangu wa kazi humu ndani usinione mjinga. Naweza kukufukuza na kumpa mtu mwingine muda wowote ule. Kwahiyo tafadhari usinipande kichwani" Rola alifoka vilivyo.
Sikuwa na namna zaidi ya kumsalimia Hussein kisha huyo nilirudi ndani, nikimuacha Rola na yule mwanaume wakibadilishana mate taratibu kabla ya kuagana na Hussein aliondoka.
Nifollow Instagram kwa jina la Burudani lazima ziendelee na huko pia.