DO YOU LOVE ME 04 (02)
LOVE IS BLIND
Tulifanikiwa kumpumzisha Mr Taz katika nyumba yake ya milele lakini katika upande huu wa mazishi, Rola hakujihusisha kabisa. Alikuwa akifanya mambo yake, mtu wa kutoka na kuingia pale nyumbani. Watu wote walimshangaa, naye hakujali hivyo. Aliona yupo sahihi kusherehekea kifo cha adui yake.
Jioni moja baada ya mazishi kupita ilikuwa kama wiki mbili hivi mbele. Rely alinitaarifu kupatikana kwa Mama yake, tulienda na kumkuta kweli Mama Rely akiwa chizi wa kutema tema mate hovyo. Vile ambavyo Rola alikuwa, ndivyo ambayo na yeye alikuwa hivyo.
Mama Rely alikuwa amepungua mwili sio kawaida, amekondeana na hata ule m-shape wake haukuwepo kabisa. Alikuwa kama akiona watu wamekaa makundi, anawarusha mawe. Akiona maji katika kopo anaokota na kunywa. Maskini! Maji mengine hayakuwa maji bali ni mkojo ila kutokana na hali yake, hakujua hilo.
Basi, tulishirikiana na watu wengine kisha tulimbeba na kumpeleka hospital. Madaktari walitusaidia kumpa huduma kadhaa, Rely aliumia sana.
"Siamini kama Mama yangu anateseka hivi. Siamini kama mwanamke aliyenilea na kunitunza kwa muda wote anateseka na kunywa maji machafu. Mama yangu amekuwa chizi kweli?" Sauti ya kitetemeshi iliyojaa maumivu makali ilimtoka msichana huyu.
"Pole sana, tusiache kumtibia. Mungu ametupa mtihani huu sababu tunaumudu. Otherwise, asingetupatia"
"Samahani! Nawahitaji" Lilikuwa sauti la Daktari ambaye alisimama nyuma yetu.
Wote tukawahi katika chumba chake ili kumsikiliza alikuwa anataka kusema nini?
"Mama alishawahi kuugua ugonjwa wowote utotoni kwa muda mrefu?" Daktari aliuliza.
"Sijawahi kupata hiyo taarifa, kwa kifupi hakuwahi kuugua"
"Mh! Kwa namna ambavyo Mama anaonekana basi ni ngumu sana kwake kupona. Mama atabakia katika hali hii kwa muda wote. Muhimu kwa hivi sasa kumpeleka katika kituo cha watu wa aina hii"
"Daktari hakuna njia kweli?"
"Nitakuongopea binti, unaweza kuzunguka kila sehemu lakini hakuna hospital ambayo inaweza kumtibia Mama yetu" Daktari alisisitiza.
Nilimuona Rely akipoteza matumaini kwa taarifa hii. Moyoni akawa na shimo la maumivu ambalo alishindwa kulifukia. Alidondosha machozi lakini hakuwa na namna nyingine zaidi ya kuuchukua ukweli ule na kuufanyia kazi.
Mama Rely sasa hivi ni chizi, tena chizi haswa. Mali alizozitaka kwa mabavu na uchawi ziligeuka kuwa mateso kwake, ama kwa hakika usimfanyie mtu ubaya kwani una tabia ya kurudi na unaporudi unarudi kwa kasi sana.
Tulirudi naye nyumbani na kuishi naye pale lakini sintofahamu ikaibuka baina ya ndugu wawili. Wakati Rely akitaka kuishi na Mama yake, ndio muda ambao Rola alikuwa hataki hata kusikia kuhusu Mama Rely kuishi pale kwake.
"Nimesema mtoeni anachafua nyumba yaani kila sehemu imejaa mate. Kama ana mimba si aende akajifungulie huko hospital sio hapa" Rola alifoka akiwa anamsukuma Mama Rely ambaye alidondoka chini.
"Rola, kwanini unamsukuma Mama? Amekukosea nini?"
"Alichokinikosea unakijua na kama hukojui basi utakijua. Kwa sasa mtafutieni makazi ila sio hapa. Siwezi kuishi na mtu ambaye ameondoa maisha ya Baba yangu, maisha ya Mama yangu. Mtu ambaye aliniroga ili achukue mali. Nimesema atoke"
"Sawa, Rola tuseme kwamba Mama anatoka. Swali ni je, tunampeleka wapi? Kumbuka huyu ndio alikulea wakati wote ulipokuwa chizi. Kumbuka hilo licha ya mabaya ambayo amekufanyia lakini atabakia kuwa Mama yangu"
"Bwana sina muda wa kurejea matukio yatakayoniumiza kikubwa nimesema ondoa hii mbwa hapa nyumbani kwangu. Kwani bila kuwaua wazazi wangu uandhani yeye angenilea? Si tamaa ya mali ndio ilimfanya auwe wazazi wangu? Sasa toeni hiyo mbwa sitaki iona hapa"
"Rola unamuita Mama yangu mbwa kweli?"
"Ndio, ni mbwa tu te..." Rola hakumaliza kuzungumza, nilimpiga kibao kimoja cha kumkumbusha kama anachoongea sio sahihi kisha nilimfokea
"Mtu gani usiyepima utu wako kwa ndugu yako? Kama wazazi wake walikutesa, kwanini ufikie hatua hii? Wapi unaenda Rola? Mbona unataka tuanze kujilaumu kwanini tulikuwa SULEIMAN kwako? Be humble bhana"
"Oh! Kumbe mnataka kuuona upande wangu wa pili si ndio? Mnataka kunijua vizuri. Ok, subirini" Rola alizungumza kisha aliondoka na kuelekea chumbani ambako alikaa kwa sekunde kadhaa na alipotoka alitoka na mabegi yetu.
"Kila chenye mwanzo kinakuwa na mwisho. Ahsanteni kwa msaada wenu katika maisha yangu, inatosha. Mnaweza kwenda kujitegemea huko mbeleni" alizungumza Rola kwa hasira sana huku akitutupia mabegi yetu. Alikuwa tayari kutufukuza, alikuwa tayari kutuhamisha pale nyumbani iwe kwa lazima ama hiyari yetu..