EPS 2 SIMULIZI;MCHEPUKO WA RAIS
SIMULIZI;MCHEPUKO WA RAIS
________________________________
CHAMA HURU MEDIA
SEHEMU ILIYOPITA.....
Matukio ya Sehemu iliyopita,Gray ambaye ni Bwana harusi amemuua mke wake Leyla masaa machache baada ya kufunga ndoa yao,Askari polisi wakaanza kumtafuta kila kona ndani ya hoteli waliyokuwepo lakini hawakufanikiwa kumpata ingawaje walitumia mfumo wa CCTV kamera.
Maswali yalikuwa mengi sehemu iliyopita,kwanini Gray amemuua mke wake Leyla..! Na imekuwaje askari polisi wafike eneo la tukio mapema Sana?.
Vilevile tuliona jinsi gani Maumivu na machungu ya Baba Leyla kumpoteza mtoto wake akajikuta akitaka kwenda kumpiga Mama yake na Gray aliyekuwa anahojiwa na askari polisi..
SONGA NAYO.....
Baba Leyla akaunyenyua mkono juu akitaka kumpiga mama Gray,endapo ngumi aliyoikunja ikimpata Mama Gray lazima atapatwa na maumivu makali,lakini kwa bahati nzuri mkono wa Baba Leyla ukazuiliwa na askari polisi mmoja aliyewahi kabla Baba Leyla hajafanya alichokikusudia.
"Baba naomba utulie" alisema Askari polisi huku akiwa ameushika mkono wa Baba Leyla.
"Niachee...niache nimuue huyu mjinga,mwanae kaniulia mwanangu kwanini nisimuue,hee...!namuua" (Baba Leyla akaendelea kulalama)
Askari polisi aliyekuwa anachukua maelezo kwa mama Gray akasema
"Mzee tunakuheshimu Sana,endapo ukiendelea usumbufu utaenda kunyea ndoo" (utaenda jela)
Baba Leyla akamtazama Askari polisi yule kwa hasira,alitamani kumpiga lakini hawezi kushindana na mamlaka,Baba Leyla akamtazama mama Gray ambaye anatokwa na machozi, hakujali hilo,akatupa macho kwa mke wake akawaona wanawake watano wakiwa wamemzunguka mke wake wakimpepelea,Mama Leyla ameshindwa kusitahimili taarifa za kuuawa kwa mtoto wake Mpaka akajikuta akipoteza fahamu(kuzimia).
Baba Leyla akatumia sekunde saba kutazama Pande zote za ukumbi ambao ulikuwa unatakiwa kutumiwa na mtoto wake ,lakini imekuwa Kama ndoto kwake kumpoteza mtoto wake wa pekee.Baba Leyla akaanza kutokwa na machozi,alishindwa kabisa kuvumilia kinachoendelea.
Askari polisi wa kwanza "pole Sana Mzee wangu,nikuhakikishie kwamba muuaji atakamatwa hawezi kwenda sehemu yeyote ile"
Askari wa pili akiwa ameshika kalamu na karatasi "Mzee wangu naomba ujipatie muda wa kutulia ili usije Fanya maamuzi mabaya, na ukiendelea kutoa vitisho kwa mama huyu ,tutakukamata bila kujali heshima yako uliyonayo nchini Tanzania"
Baba Leyla akatoa kitambaa (leso)akajifuta machozi kisha akawaacha Askari wale wawili wakiwa wamesimama na mama Gray,ukumbi ambao muda mchache uliopita ulitumika kufurahia uwepo wa wanandoa wapya umegeuka kuwa ukumbi wa maombolezo.Ndugu,jamaa na marafiki wa familia ya Leyla walikuwa wanahuzuni kubwa ,lakini pia waliingiwa na chuki dhidi ya familia ya Gray.
**
Baba leyla anafahamika kwa Jina la Jamal Ismail Omar,ni miongoni Mwa majina maarufu nchini Tanzania, huyu ni mfanyabiashara mkubwa anayemiliki viwanda vya utengenezaji wa vinywaji pamoja na mabasi yanayosafirisha abiria na mizigo mikoa mbalimbali nchini.
Jamal Ismail Omar,asili yake ni kutoka Somalia,alikuja Tanzania miaka therathini na tatu iliyopita kwa ajili ya kufanya biashara,akapapenda na kuanzisha makazi ya kudumu ndani ya mkoa wa shinyanga wilaya ya kahama.
Sophia mihayo,ni mama yake mzazi na Marehemu Leyla,huyu ni Mtanzania kutokea mkoani singida,walikutana na Jamal wilayani kahama,mkoa wa shinyanga. Mahusiano yao yalizaa matunda wakampata Leyla ambaye ni mtoto wao wa pekee.
Leo hii mtoto wao wa pekee ameuawa na mume wake siku ya harusi,Maumivu wanayoyapitia Jamal na Sophia hayakuwa na kifani,Mama Leyla ameshindwa kustahimili taarifa za kumpoteza mtoto wake amejikuta akipoteza fahamu,wageni waalikwa wamepata jukumu la kumpepea Sophia.
**
Upande wa pili kwa inspekta Alexander Dickson alikuwa nje ya hoteli na askari wengine wakiendelea kufanya uchunguzi wa kina ,walitumia Mpaka mbwa waliofundishwa mafunzo ya kijeshi lakini hawakuweza kumuona Gray.
Inspekta Alexander akiwa anamulika mulika ukutani akasema
"Hii inashangaza Sana,muuaji ameelekea wapi baada ya kufanya tukio..!"
Askari mmoja akajibu.
"Kwani mkuu ilikuwaje ukafahamu Kama hapa kuna mauaji yametokea?"
Inspekta Alexander akajibu
"Kuna mtu alinipia simu wakati nikiwa ofisini kwangu"
Askari akasema
"Vipi Kama aliyepiga simu akawa ametuchezea huu mchezo..?"
Inspekta Alexander akamtazama askari wake
"Afande Morice, kazi yetu ni kufanya uchunguzi wa kina Mpaka tupate mwafaka wa haya yote,majibu yetu yatapatikana endapo tukimpata muuaji,kuhusu aliyepiga simu naomba tuachane nayo kwa sasa,sawa?"
"Sawa mkuu"
Inspekta Alexander akamuacha afande Morice aendelee kusaidizana na askari wenzie kuchunguza kuta za hoteli ili Kama muuaji ametoka ndani ya jengo la hoteli wafahamu.
Ndani ya mjengo wa hoteli kubwa ya kifahari, askari polisi walikuwa wanaendelea kufanya uchunguzi wao kila kona,waliingia Mpaka stoo na jikoni lakini jitihada zao hazikuzaa matunda.
Gray ametoka kufanya tukio la mauaji kwa mke wake na cha ajabu haonekani alipoelekea,Askari polisi waliumiza vichwa vyao usiku wa Leo kwa sababu wanamtafuta mtu ambaye hawafahamu yupo wapi,kwa wakachokifanya askari polisi ni Kama mchezo maalufu kutafutana unaochezwa na watoto wadogo.
**
Inspekta Alexander Dickson akasogea eneo la waandishi wa habari waliokuwa wamesimama kando ya geti kuu la kuingilia hotelini,walipomuona wakamsogelea huku wakiwa wamebeba vifaa vyao vya kurekodia sauti na picha mjongeo(video).
Askari polisi watatu wakasogea karibu na inspekta Alexander kwa ajili ya kumpatia ulinzi na usalama dhidi ya waandishi wa habari.Maswali ya waandishi wa habari yakaanza kuulizwa,mwandishi mmoja wa kike akasikika akisema.
"Kwa majina naitwa Caren jumanne,natokea katika Gazeti la Mtanzania,nilikuwa naomba kufahamu ni hatua ipi ambayo jeshi la polisi limefika baada ya tukio la mauaji kutokea ndani ya hii hoteli?"
Inspekta Alexander Dickson akajibu
"Hatua tuliyofikia siyo mbaya Sana,wala siyo nzuri Sana ,naomba mnielewe tu,kwa sasa siwezi kuongelea kinachoendelea Mpaka pale tukikamilisha taratibu zote,lakini niwahakikishie tu,mtuhumiwa atakamatwa na ataadhibiwa kwa mujibu wa vifungu vya sheria ya Tanzania" Inspekta Alexander hakutaka kuendelea kufanya mahojiano tena na waandishi wa habari,akageuka na kurudi kuendelea kufanya uchunguzi.
Waandishi wa habari walitamani kuuliza maswali mengi kwa inspekta Alexander lakini hawakupatiwa muda huo tena kwa sababu Alexander ana uchu wa kumpata muuaji,na hii ndio sifa pekee inayomtofautisha inspekta Alexander na wapelelezi wengine waliopo nchini Tanzania, yeye hupenda kulitafutia ufumbuzi tatizo lililopo mbele yake mpaka pale afanikiwe.
Waandishi wa habari wakaanza kurusha matukio mbalimbali yanayojili pamoja na alichokisema inspekta Alexander Dickson muda huu,kila mwanahabari alikuwa anajitahidi kurusha haraka kwenye chaneli yake anayofanyia kazi.
**
(Dar es salaam; 09-50usiku)
Saa Tatu na dakika hamsini usiku,vyombo mbalimbali vya habari vilianza kuripoti taarifa ya habari kuhusu tukio la mauaji ya Leyla ambaye ni Binti wa pekee katika familia ya mfanyabiashara mkubwa nchini Tanzania.
Kwenye sebule moja ya kifahari ambayo inavito vya thamani,alionekana mwanaume mmoja mwenye umri wa makamo ya miaka arobaini akiwa anatazama runinga,alivalia bukta nyeusi pamoja na tisheti nyeupe.
Sura yake ilishamili tabasamu baada ya kusikia sauti ya msomaji wa taarifa ya habari.
“Shinyanga” Ndivyo alivyoanza msomaji wa taarifa ya habari katika kituo kimoja kikubwa cha runinga.
*“Jeshi la polisi mkoani shinyanga linapenda kuujulisha umma juu ya tukio la mauaji lililotokea wilayani kahama ndani ya hoteli ya Malunga,tukio hili linamhusisha mtoto wa pekee katika familia ya mfanyabiashara Jamal Ismail anayefahamika Kama Leyla,kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa Inspekta Alexander Dickson ambaye ni mkuu wa kitengo cha upelelezi mkoani shinyanga,amesema,Mtuhumiwa wa kifo cha Leyla ni mume wake aliyefunga naye ndoa siku ya leo,Mtuhumiwa anafahamika kwa jina la Grayson Mwailubi.Jeshi la polisi linawaomba wananchi kutoa taarifa pale ambapo mtuhumiwa akionekana uraiani"*
Msomaji wa taarifa ya habari ya dharura akaweka kituo na kuruhusu runinga kuonesha video ya mahojiano yao na inspekta Alexander Dickson.
Anayetazama runinga peke yake sebuleni akazidi kuachia tabasamu, haikuwa inafahamika ni nani na kwanini ameachia tabasamu baada ya kupokea taarifa zile.
Mwanaume yule akachukua simu yake aliyokuwa ameiweka mezani, akabofya batani mara kadhaa ,akatafuta namba ya mtu anayetaka kumpigia,akapiga.
Simu ikaanza kuita,baada ya sekunde kadhaa kupita simu ikapokelewa, Mwanaume Yule akasema.
"Kazi imeisha" Upande wa pili wa simu haukusikika,alipomaliza kusema maneno Yale akakata simu kisha akazima runinga,moja kwa moja akaanza kupiga hatua kuelekea chumbani kwake.
Maisha ya mwanaume huyu ni mazuri sana,nyumba yake inakila kitu kwa mahitaji maalumu ya mwanadamu,sofa ,meza na viti vyote ni vya kisasa zaidi.
Ukutani kulikuwa na picha ya huyu mwanaume akiwa amevalia suti nyeusi,tai ya bendera ya Taifa pamoja na saa ya gharama,chini ya ile picha kulikuwa na maandishi madogo yakiwa yana maana Fulani.
**
Upande wa pili kwa Baba Leyla (Jamal Ismail Omar),akasogea mbali kidogo na askari polisi kisha akatoa simu yake aina ya iPhone 15,akabonyeza kitufe cha kutunza namba halafu akachagua namba anayotaka kuipigia, Jamal Ismail akaipigia namba moja aliyoisevu 'Mr P'.
Simu ikapokelewa upande wa pili,baada ya simu kupokelewa Jamal Ismail akaiweka sikioni huku akiwatazama askari polisi ambao walikuwa bize kulinda amani kwa wageni waalikwa waliokuwa wamehudhuria harusi ya Bwana Gray na marehemu Leyla.
Baba Leyla (Jamal Ismail) akazungumza kwa sauti ya chini na iliyojaa hisia ya maumivu ndani yake.
"Nadhani kazi yako unaifahamu"
Upande wa pili wa simu sauti ya mwanaume ikajibu.
"Ndiyo mkuu"
Jamal Ismail akakata simu na kuirudisha mfukoni,akashusha pumzi 'huuuuu'.
Inspekta Alexander Dickson akaingia ukumbini huku akiwa ameongozana na askari watatu pamoja na wahudumu wa afya wawili ambao wamekuja kwa lengo la kumpatia huduma mama Leyla.
Wahudumu wa afya wakasogea mpaka kwa mama Leyla ambaye kapoteza fahamu, wakawaondoa wamama wote waliokuwa wamenzunguka mama Leyla,wakaanza kumpatia huduma ya kwanza.
Inspekta Alexander na askari watatu wakaanza kumsogelea Baba Leyla huku sura zao zikionekana kuwa za mkazo maana walimtazama kwa macho makavu Sana(kukaza sura),Baba Leyla akashindwa kuelewa Kwanini askari polisi wanamsogelea,alipotupa macho mkononi kwa insp.Alexander Dickson akamuona akiwa ameshika pingu,hofu ikaanza kumtanda Baba Leyla kila alipowaona askari polisi wanaomsogelea eneo alilosimama.
Kwa sauti ya chini Baba Leyla akajisemea
"Au wamenigundua nini?" (akavuta pumzi)
Inspekta Alexander Dickson na askari wenzake watatu wakafika aliposimama Baba Leyla, mapigo ya moyo ya baba Leyla yalikuwa yanamwenda mbio,kuna jambo ambalo baba Leyla analificha na hatamani askari polisi walijue.
Baba Leyla na Insp.Alexander Dickson wakatazamana machoni,ukimya baina yao ndio uliendelea kutawala,Baba Leyla anahofu ndani yake lakini inspekta Alexander Dickson anamtazama Baba Leyla kwa macho ya kiudadisi zaidi huku mkononi ameshika pingu.
.......
Soma full story kwa sh 1000
Njoo WhatsApp 0781858056
Makala nyingine zinazocheza na ladha yako
Mapendekezo haya yanatokana na kile unachosoma sasa + Endelea kugundua zaidi


















Maoni